BINTI anayeshikilia Tuzo ya Mwigizaji Bora wa Kike ya Ziff 2013, Elizabeth Michael maarufu Lulu ameweka wazi kuwa amepata mchumba na kwamba taratibu za kujitambulisha na mahari vitafuata baadaye.
“Unajua mimi ni binadamu na ili nitulie na kujiepusha na majanga, ni vyema kuwa na mpenzi mmoja  mwaminifu, anayenijali mimi na kazi yangu hapo nitasimama na kusema kwamba nimepata sehemu ya kutulia na kuanza maisha mapya ya uhusiano na ndoa,” anasema Lulu.
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiom6JK6aQ9PN8Kac72Gdqsn4-x10lBTuGzTor6EruNMrqB1_qy5aMNgk8BqF_B3zL0tD8E1bAcNe86T2EJNvXCuiNDemKOh-bEkJJ8jHP1Cja5bXaMcc0huubKtNrvUQ9aigIXrJAOIR0_/s1600/165523_187953291234765_100000602853028_580725_7351981_n.jpg

Hata hivyo anasema yeye na mchumba huyo (ambaye hakutaka kuweka wazi jina lake) wana mikakati mingi katika kuyafikia maisha ya uhusiano yaliyo wazi na yenye baraka za wazazi.
“Siwezi kukutajia jina kwa sasa itafika wakati atajulikana tu, hata hivyo bado hatujafikia hatua muhimu ikiwa ni pamoja na kujitambulisha kwa wazazi na masuala ya mahari na ndoa. Vitu kama hivi vitafanyika baadaye mwaka huu, hata hivyo wazazi wangu sidhani kama watakuwa na pingamizi katika hili kwani mimi ni mtoto wa kike na nimekua sasa,” anasema.
Kuhusu Mama Kanumba Lulu anasema: “Huyu ni mama yangu hana tofauti na mama Lulu hivyo anajua kila kitu na amenipa baraka zake zote, yaliyopita si ndwele kinachotakiwa ni kuganga yajayo, namshukuru mama kwani amenionyesha upendo wa kweli na kunishauri katika maisha, bila yeye nisingekuwa na ujasiri nilionao sasa.
“Mama Kanumba ni rafiki yangu wa ukweli, ana mapenzi mazito sana kwangu amekuwa mstari wa mbele kunishauri na kunipa mwongozo wa maisha ni nini na wapi nilipokosea na natakiwa kufanya nini ili kuwa na maisha yaliyonyooka,” anasema mwigizaji huyo anayetamba na filamu ya Foolish Age.
Lulu mwenye miaka 19, anasema haikuwa rahisi kwake kufikiria kutulia kiuhusiano ila amepewa mwongozo bora unaomfanya afikirie kufanya hivyo kwa sasa.
“Mimi ni binti na kama ujuavyo nina mapenzi yangu moyoni, si kazi rahisi kuamua kwa sasa lakini nimepewa mwongozo bora na kuona nini natakiwa kufanya. Kama binti napaswa kuzingatia maadili, mimi ni kioo cha jamii, inafika hatua inabidi niishi katika maadili hilo ndilo ninalolifanya sasa.”
Anasema wazazi wake wamempa baraka zote kuhusu uhusiano wake wa sasa: “Wazazi wangu sasa wanafahamu kwamba nimepata mchumba, kwa kweli wamenipa baraka zao zote, pande zote hata Mama Kanumba. Nimekua sasa na mimi nina uamuzi wangu, ni vema kuangalia ninataka nini lakini kikubwa wananishauri.”
Anasema wazazi wake hawakubali kila anachokitaka: “Sina wazazi wa kukubali kila ninachokitaka ila nina wazazi waelewa, wenye kuangalia jambo kabla hawajaniambia sasa unaweza kuendelea, mama yangu ni mkali sana, hana mchezo hasa pale anapoona kwamba nayumba kimaisha,” anasema Lulu.
Kuhusu tetesi zilizoenea kwamba ana uhusiano na msanii wa hip hop Young Dee, Lulu alikana na kusisitiza kwamba hajawahi hata kuwa na ukaribu na msanii huyo.
“Nashangaa taarifa hizo watu wanazitoa wapi na mpaka leo nashangazwa na uvumi ulioenea kwamba tulifumaniwa, usiku ule nilikuwa sehemu nyingine tofauti kabisa, ukweli ni kwamba sijawahi kuwa na ukaribu na Young Dee, wala hata kumfikiria kama ninaweza kuwa na uhusiano naye. Bado, hatulingani kwa kweli,” anasema.
TUPE MAONI YAKO HAPA:
LIKE PAGE YETU ILI UPATE HABARI ZAIDI

0 comments:

Post a Comment